Copyright @ 2007 Dullonet.com. All Right Reserved
JINAMIZI bado linauandama uongozi wa zamani wa Shirikisho la Ngumi za Ridhaa Tanzania (BFT), chini ya Rais Alhaj, Shabani Mintanga, baada ya kutuhumiwa kutumia madaraka vibaya.
Mintanga ambaye yupo rumande tangu mwaka jana akituhumiwa kula njama ya kusafirisha dawa za kulevya nchini Mauritius huenda akapandishwa tena kizimbani kujibu shtaka la kuuza gloves zinazodaiwa ni mali ya BFT pamoja na aliyekuwa makamu wake Christopher Mutarubukwa ‘Chris Mutta’.
Akizungumza jana, kiongozi mmoja wa BFT ambaye hakupenda kutajwa jina lake kwa madai kuwa si msemaji, alisema viongozi hao waliomaliza muda wao kwa kujiuzulu kutokana na kashfa ya dawa za kulevya huenda wakafikishwa mahakamani kutokana na suala hilo.
Alisema wanashangaa kukabidhiwa gloves chache wakati ipo misaada mingi kutoka Shirikisho la Ngumi la Kimataifa (AIBA), inayokuja kila mwaka; halikadhalika vifaa na misaada kutoka Kampuni ya Hamka na Watanzania wanaoishi Amerika ya Kaskazini.
Kiongozi huyo alidai kuwa gloves hizo zilizokuwa kwa Mintanga na Mutta, zipo na zinauzwa kwenye duka moja lililopo Kariakoo, Mtaa wa Msimbazi karibu na kituo cha polisi.
“Tunafanya mawasiliano na AIBA, pamoja na Shirikisho la Ngumi Afrika (ABC) ili tupate uhakika ni kiasi gani walichokuwa wakitumiwa na tupeleke hesabu kwa mkaguzi mkuu wa Serikali ili tuweze kuwafungulia kesi ya kutumia madaraka vibaya,” alisema.
Kabla ya kupatikana kwa uongozi mpya chini ya Rais Joan Minja, uongozi uliokuwepo chini ya Mintanga ulijiuzulu mwaka jana kutokana na kashfa ya kusafirisha dawa za kulevya nchini Mauritius.
.
.
Posted by Dullonet: 24.03.2009
Source: Mwandishi Maalum